Historia ya Ushirika wa Moravian Kinondoni

Utangulizi
Historia ya Ushirika wa Kinondoni inaanza kwa kuwatambua baadhi ya wakristo waliojitoa mhanga kuratibu/kukusanya waumini na baadae kuanzishwa kwa kituo ambacho leo kinajuikana kama Ushirika wa Kinondoni. Kazi hiyo ilifanywa na ndugu, Benjamini Mwalwisi, ndugu John Mwakyembe na ndugu Edwini Mwaipopo (ambaye alikuwa ni Mwalimu wa Kwaya). Kiongozi wao alikuwa ni ndugu Benjamin Mwalwisi. Kazi kubwa ilikuwa ni ya uinjilisti wa kwaya iliyokuwa ikiongozwa na Mwalimu Edwini Mwaipopo. Baadaye idara zingine za kanisa zilianzishwa na ziliongozwa na hawa wafuatao:
- Idara ya kwaya iliongozwa na ndugu Edwini Mwaipopo
- Idara ya Umoja wa Wanawake iliongozwa na T. Somola (Mrs Mwalwisi)
- Idara ya vijana iliongozwa na Ndugu N.T Mwasikili
- Pamoja na Idara ya Shule ya Jumapili.
Mahali Pa Kuabudia : Ibada Zilianza Rasmi Mwaka 1983
Kwa kutumia majengo ya shule ya msingi Kumbukumbu ambayo uongozi wa shule hiyo uliombwa kutumia madarasa ya shule hiyo kwa ajili ya kufanyia ibada. Kituo hiki kilipokuwa kinaanzishwa kilikuwa chini ya ushirika wa magomeni Moravian. Baada ya muda mfupi kupita uongozi wa shule na msikiti uliokuwa karibu na shule hiyo ukasitisha kutumia majengo ya shule hiyo kwa ajili ya ibada
Hivyo uongozi wa kanisa uliomba kufanyika ibada zake katika shule ya msingi Kinondoni ambapo walikubaliwa kutumia madarasa ya shule hiyo na bwalo la chakula la wanafunzi . Ibada hizi ziliendeshwa hapo shuleni kwa muda mrefu.
Ushirika
Kituo hiki kilipata hadhi ya kuwa ushirika kunako yarehe 24 Februari 1985. Ndipo ushirika ulifunguliwa rasmi chini ya Mchungaji Peter Joel Kabigi( kwa sasa ni Marehemu).
Changamoto Mwaka 1983 – 2000
Kama tulivyokwisha kusema huko nyuma ushirika haukupata kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa kanisa kwa muda wa miaka kumi na saba(17) uliendesha ibada zake katika sehemu mbalimbali maeneo ya kinondoni na Mwananyamala ambazo ni;-
- Shule ya msingi Kumbukumbu
- Shule ya msingi Kinondoni
- Viwanja vya mkwajuni
- Eneo la Mzee wa Kanisa – Mama Anna Kibinga
- Ukumbi wa A.E.E
- Kanisa la Presbetarian
- Ukumbi wa Biafra
Kazi Zilizofanyika Na Ushirika:
- Utafutaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa kanisa
- Uinjilisti katika maeneo yanayauzunguka ushirika wetu
- Kutoa elimu kwa kuwapeleka shule wainjilisti wa kanisa na kutoa huduma mbalimbali za kimwili na kwa kijamii.
Utekelezaji Wa Kazi Hizo:
Juhudi mbalimbali zilifanyika na wakristo walishirikiana na wachungaji waliopitia katika ushirika huu katika kutafuta viwanja kwa ajili ya ujenzi wa kanisa. Katika juhudi hizo tulifanikiwa kupata kiwanja eneo la mkwajuni toka serikalini ambacho kanisa lilitapeliwa na kuuziwa mtu mwingine. Washirika hawakukata tama juhudi ziliendelea kutafuta maeneo mengine .
Tulifanikiwa kupata nyumba eneo la Mwananyamala karibu na hospitali. Nyumba ambayo ilikuwa inauzwa, kanisa liliamua kuinunua nyumba hiyo kwa gharama ya Tsh 800,000/- kwa lengo la kuibomoa na kujenga nyumba ya kuabudia. Juhudi za kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi zilipokuwa zikiendelea mama mwenyenyumba aliyetuuzia kanisa akafariki. Baada ya msiba huo watoto wa marehemu wakafungua kesi mahakamani kupinga ununuzi wa nyumba hiyo walidai kwamba wao ndio warithi wa nyumba hiyo. Kesi ikaendelea Mahakamani ilionekana kwamba mmiliki halali wa nyumba ni aliyekuwa ameandikishwa kwenye mirathini motto wa marehemu ambae anaishi nchini Kenya . Hivyo mahakama ikaamua kwamba kanisa halina haki katika ununuzi wa nyumba hiyo. Hivyo Kanisa likapoteza uhalali wa kumiliki nyumba hiyo.
Juhudi hizo hazikuishia hapoi washirika waliendelea kutafuta maeneo mengine kwa kusudi hilohilo. Tukafanikiwa kupata viwanja viwili karibu kabisa na shule ya msingi kinindoni , viwanja hivyo vilikuwa vinamilikiwa na ndugu O. Mwaulanga ambae aliamua kuliuzia kanisa . Baada ya uchunguzi kanisa liliamua kuvinunua viwanja vyote viwili kwa jumla ya Tsh. 20,000,000/-
Baada ya malipo hayo kufanyika zilianza juhudi za kusafisha eneo hilo la viwanja kwa ajili ya ujenzi wa kanisa. Ndipo serikali ikasimamisha kazi hiyo ya ujenzi kwani viwanja hivyo vilikuwa ni vya shule ndio waliokuwa wamepewa umiliki wake. Hivyo ushirika ukajikutakwamba umetapeliwa na Ndugu O. Mwaulanga.
Ushirika ukaamua kumfungulia mashtaka mahakamani O.Mwaulanga . Mahakama iliamua kwamba ndugu Mwaulanga arudishe fedha alizochukua kwa kanisa.
Baada ya utapeli huo washiriks walivunjika moyo kwa washirika . Baraza la wazee wa kanisa liliamua kutafuta nyumba na kuinunua kwa gharama zao wenyewe bila kuwashirikisha washirika nyumba hiyo ilipatikana eneo la msisili ambayoilinunuliwa kwa ghrama ya Tsh 6,000,000/-.Baada ya ununuzi huo ndipo baraza la wazee liliwashirisha washirika na kuweza kuhamia katika nyumba hiyo ambayo ilifanyiwa ukarabati na kuweza kuendesha ibada katika nyumba hiyo( katika eneo hili tunapenda kuwapongeza baraza la wazee na ndugu wafuatao:- Erasto Kasekwa na Bibi Mary Mbogo wawili hawa walituongoza katika mapambano ya ununuzi wa nyumba hiyo chini ya Mchungaji O. Ndile) 2001: tar. 24 Februari 2001.
Hapa ukawa ni mwanzo kukaa chini kuweka mikakati kuanza kujenga kanisa hili sasa. Kwa uwa eneo hili lilikuwa dogo kwa ajili ya ujenzi wa kanisa na nyumba ya kuishimchungaji, juhudi ziliendelea kutafuta eneo linguine kwa ajili ya kujenga nyumba ya kuishi wachungaji , tulifanikiwa kupata nyumba toka kwa mkristo mwenzetu ambaye aliamua kuliuzia kanisa nyumba yake kwa gharama ya Tsh 15,000,000/- ushirika ulinunua nyumba hiyo ambayo ndipo wachungaji wetu wanaishi sasa.
Uinjilisti Nje Ya Ushirika;
Pamoja na kutokuwa na nyumba ya kuabudia wakati huo ushirika uliendelea na kazi ya uinjiristi katika maeneo hayo kwa ajili ya ujenzi wa makanisa maeneo hayo ni;
- Eneo la Mwenge ambalo sasa ni ushirika
- Eneo la Kawe ambalo sasa ni ushirika
- Eneo la Boko ambalo sasa ni ushirika
- Eneo la Mbezi Beach ambalo sasa ni ushirika lakini hatukununua kiwanja huko.
Elimu Kwa Wainjilisti
Ushirika ulimpeleka Mwinjilist L. Mwaseba kusoma masomo ya uinjilist ambaye baadae alichukuliwa na Jimbo na sasa ni Mchungaji (Hili ni tunda letu) . Ushirika uliendelea na kazi ya kumsomesha Mwinjilisti F. Chimtembo ambaye amechukuliwa na Jimbo kwa ajili ya masomo ya kichungaji na sasa ni Mchungaji.
Wachungaji Waliowahi Kutoa Huduma Katika Ushirika Huu
- Peter Joel Kabiji............................................................Mwaka 1985 – 1988
- Nelson Kagisya.............................................................Mwaka 1988 – 1993
- Mch . Peterson Lwinga..................................................Mwaka 1993- 1995
- Joseph Lwinga..............................................................Mwaka 1995- 1996
- Lugano Mwakanyamale.................................................Mwaka 1996- 1998
- Christopher Mwenga.....................................................Mwaka 1998 – 1999
- Owden Ndile................................................................Mwaka 1999 – 2005
- Mch Alli Ambukege.......................................................Mwaka 2005 – 2007
- Mch .Sauli Kajula..........................................................Mwaka 2007 - 2010
- Israel Kabuka...............................................................Mwaka 2010- 2013
- Kiporoza (KKKT)...........................................................Mwaka 2014- 2016
- Kamati ya watu sita......................................................Mwaka 2016- 2018
- Gentleman Mwansile....................................................Mwaka 2018 hadi sasa
Shukurani
Tunatoa shukurani kwa wote ambao Mwenyezi Mungu aliwatumia kwa kipindi hiki kigumu kwa kutoa misaada, ushirikiano na ushauri ili kufanikisha kazi ya kanisa iendelee kufanyika. Pia kwa wote walioturuhusu kutumia maeneo yao kuendesha ibada kama ilivyotajwa hapo juu.
Shukurani za pekee ziende kwa viongozi wa kanisa letu waliokuwa bega kwa bega pamoja na wachungaji waliotumika katika kipindi hiki. Mwisho shukurani ziwafikie wakristo wote wa ushirika huu ambao walishikamana na kutokata tamaa kwa kipindi hiki mpaka tumefika hapa tulipo sasa.